MASHINDANO YA UMISETA NGAZI YA WILAYA YAFUNGULIWA RASMI KARAGWE DC
Leo tarehe 03/06/2025 Mashindano ya Umoja wa Michezo Sekondari Tanzania (UMISETA) kwa mwaka 2025 yamefunguliwa rasmi katika Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe kwenye kiwanja cha michezo cha Bashungwa.
Akifungua Mashindano hayo, Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe Bi. Henrietta William ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya jamii amewataka Wanafunzi wanaoshiriki katika mashindano hayo, kujituma na kudumisha nidhamu kipindi chote cha maandalizi ili watakaopata nafasi ya kuiwakilisha Wilaya kwenye mashindano hayo ngazi ya Mkoa wakafanye vizuri.
"Nitoe shime kwa Wanafunzi wote mnaoshiriki mashindano haya, mkayachukulie kwa uzito kwa sababu siku hizi michezo ni ajira na inaweza kukupeleka sehemu ambazo hukufikiria kufika, mkatuwakilishe vyema kwenye mashindano ya Mkoa kwa nidhamu na matokeo chanya ", amesema Bi. Henrietta.
Naye, Kaimu Afisa Elimu Sekondari wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe Ndg. John Bosco amesema uwepo wa UMISETA mashuleni si upotezaji wa muda bali ni nafasi nzuri kwa Wanafunzi kuonyesha vipaji vyao na kukua kitaaluma kwasababu Michezo inaimarisha Afya zao.
Kwa upande wake Afisa Michezo wa Halmashauri hiyo, Ndg. George Sebastian amesema kuwa, anamatumaini makubwa ya kushinda Mashindano hayo kwa ngazi ya Mkoa kwa sababu Wanafunzi wameandaliwa vizuri.Mashindano haya kwa ngazi ya Mkoa yanatarajiwa kufanyika Wilaya ya Muleba kuanzia tarehe 06/06/2025 katika Viwanja vya Chuo cha Walimu Katoke.
Aidha, Michezo itakayoshindanishwa ngazi ya Mkoa na Taifa itahusisha Mpira wa miguu kwa Wasichana na Wavulana, Mpira wa wavu kwa Wavulana, Mpira wa Netiboli, Mpira wa Mikono kwa Wavulana, Riadha kwa Wavulana na Wasichana, Kwaya, Ngoma na Mpira wa Meza.
KARAGWE KAGERA TANZANIA
Anuani ya posta: BOX 20 KARAGWE
Simu: 028-2227148
Simu ya mkononi: 028-2227148
Barua pepe: ded@karagwedc.go.tz ded.karagwedc@kagera.go.tz
Copyright©2017 karagwedc. All rights reserved.