KARAGWE DC YAADHIMISHA SIKU YA MTOTO WA AFRIKA.
Leo tarehe 16/06/2025 Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe imeadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika kama yalivyokua makubaliano ya
Mwaka 1991 ambapo Umoja wa Nchi za Afrika waliamua kuenzi kumbukumbu ya mauaji ya Watoto takribani 2,000 yaliyofanywa na Utawala wa Makaburu, nchini Afrika Kusini tarehe 16 Juni, 1976, wakati wa maandamano ya wanafunzi waliokuwa wakipinga mfumo wa Elimu ya kibaguzi iliyokuwa inatolewa na Utawala wa Afrika Kusini.
Akizungumza kwa Niaba ya Mkuu wa Wilaya Bi. Henrietta William ambaye pia ni Mkuu wa Idara ya Maendeleo ya jamiii wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe amesema kuwa Siku ya Mtoto wa Afrika inaikumbusha jamii kutafakari haki za watoto na kuhakikisha wanawatimizia ili kujenga kizazi chenye maadili na uwajibikaji. Pia ametumia nafasi hiyo kusisitiza umuhimu wa kuwepo kwa Baraza la Watoto mashuleni.
"Niwasihi muendeleze Mabaraza ya watoto kwasababu kupitia mabaraza hayo watoto wanapata nafasi ya kueleza changamoto wanazokutana nazo ikiwemo maswala ya ukatili kwa watoto" Alisisitiza Bi. Henrietta.
Naye, Afisa ustawi wa Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Karagwe Bi. Wokusima Kaihura amesema kuwa Maadhimisho hayo yawe ni sehemu ya tathimini ya kuona ni namna gani Wazazi wanasimama kwenye nafasi zao hasa kwenye suala la malezi na makuzi.Pia amewasisitiza wazazi kuimarisha ulinzi wa watoto wao ili kuwaepusha kwenye ukatili.
Kwa upande wake, Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji cha Muungano Mhe. Jefta Edward ameushukuru Uongozi wa Halmashauri kwa kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika kwenye kijiji cha Muungano na amewapongeza Wananchi kwa kujitokeza kwa wingi.
Hatahivyo, Kila mwaka tarehe 16 Juni Tanzania inaungana na Nchi zingine za Afrika kuadhimisha Siku ya Mtoto wa Afrika ikiwa na kauli mbalimbali zenye tija kwa ustawi wa watoto.Kwa mwaka huu Kaulimbiu ya Maadhimisho ya Siku ya Mtoto wa Afrika inasema "Haki za Mtoto: Tulipotoka, Tulipo na Tuendako.” ikiwa na lengo la kututafakarisha kuhusu upatikanaji wa haki za watoto tangu zilipoainishwa na Sera ya Maendeleo ya Mtoto mwaka 2008.
KARAGWE KAGERA TANZANIA
Anuani ya posta: BOX 20 KARAGWE
Simu: 028-2227148
Simu ya mkononi: 028-2227148
Barua pepe: ded@karagwedc.go.tz ded.karagwedc@kagera.go.tz
Copyright©2017 karagwedc. All rights reserved.